TANGAZO

TANGAZO

Ijumaa, 3 Julai 2015

Upinzani ‘walianzisha’ tena bungeni




Dodoma. Mwongozo ulioombwa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika jana ulizua kizaazaa na kumlazimisha Spika Anne Makinda kuahirisha kikao baada ya kukosekana utulivu ndani ya Ukumbi wa Bunge.
Kikao hicho kiliahirishwa muda mfupi baada ya kipindi cha maswali na majibu wakati Bunge lilipotakiwa kukaa kama kamati kumalizia kiporo cha Muswada wa Sheria ya Kuwalinda Watoa Taarifa za Uhalifu na Mashahidi wa mwaka 2015 ambao mchakato wa kuupitisha haukukamilika juzi kutokana na muda kuisha.
Ilikuwa ni kama marudio ya hali ilivyokuwa mwishoni mwa mwaka jana wakati wabunge wa upinzani waliposimama na kuweka mazingira ambayo yalizuia shughuli za chombo hicho kuendelea wakati wa kujadili sakata la escrow.
Jana, sakata hilo lilitokea baada ya Spika Makinda kuweka sharti la kutoa mwongozo ulioombwa na Mnyika aliyetaka kujua sababu za uongozi kuwasilisha miswada mitatu kwenye shughuli za jana licha ya wabunge wa pande zote mbili kuipinga kwa kuwa haina haraka.
Kutokana na majibu hayo, wabunge wa upinzani walisimama na kuanza kupiga kelele wakipinga kitendo hicho cha uongozi wa Bunge huku wakisema; “muda wa kuburuzana umekwisha.”
Hata Spika Makinda alipojaribu kuwatuliza walipiga kelele na kumfanya kiongozi huyo wa chombo cha kutunga sheria kutangaza kuahirisha shughuli za Bunge.
 Hali ilivyokuwa
Mwongozo wa Mnyika ulitokana na ratiba ya shughuli Bunge kuonyesha kuwa kulikuwa na miswada minne iliyotakiwa kujadiliwa.
Hiyo ilikuwa ni Muswada wa Sheria ya Kuwalinda Watoa Taarifa za Uhalifu na Mashahidi wa mwaka 2015 ambao ulifikia ngazi ya Bunge kukaa kama kamati kuupitisha, Muswada wa Sheria ya Petroli wa mwaka 2015, Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Mapato ya Mafuta na Gesi na Muswada wa Sheria ya Uwazi na Uwajibikaji katika Uchimbaji.
“Mheshimiwa Spika, naomba mwongozo wako kwa kutumia kanuni ya 53 (1) na (6) ambazo zinasomwa pamoja na kanuni ya 86 katika vifungu vya 1,5,6, kwamba Bunge lako limekiuka kanuni kwa kuleta hoja juu ya hoja,” alisema Mnyika.
Alipopewa nafasi ya kufafanua hoja yake, Mnyika alisema: “Tarehe 29 Bunge lako lilipokea semina juu ya miswada hii mitatu ambayo leo imeingizwa tena bungeni na wabunge kwa kauli moja, bila ya kujali itikadi za vyama, tulipinga jambo hili lakini leo tunaona mmeleta tunaomba ufafanuzi,”

Alisema na kumtaka Spika atoe ufafanuzi hapohapo kwa kuwa jambo hilo lilikuwa ni muhimu.

 Majibu ya Spika
Spika Makinda alisimama na kumtaka kwanza Mnyika kuondoa maneno ya amri kwani vinginevyo asingeweza kutoa jibu lolote kwa madai kuwa hawezi kuamrishwa.
“Ondoa maneno ya kuamrisha hapa, nasema ondoa maana nyinyi tabu yenu ni kuwa hamjajiandaa kwa shughuli hii, tena ikumbukwe kuwa tulikaa kikao cha Kamati ya Uongozi mara baada ya semina ile na Mheshimiwa (David) Silinde alikuwapo, sasa mnasemaje tena?” alisema Makinda.
Hata hivyo, kauli yake ni kama iliongeza hasira kwa wabunge wa upinzani ambao walisimama na kuanza kupiga kelele wakisema lazima miswada hiyo iondolewe.
Kuona hivyo, Makinda alisimama na kusema: “Sasa amueni ninyi maana mliomba mwongozo au amueni wenyewe sasa.”
Kelele za wabunge zilizidi kiasi cha kuibuka majibizano kutoka kwa wabunge wa pande zote na wakati huo tayari Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Bunge, Jenister Mhagama akiwa amesimama huku wapinzani wakiimba “tumechoka kuburuzwa, mnataka mafisadi kututawala.”
Ndipo Spika akasema: “Waheshimiwa wabunge, ninaahirisha shughuli za Bunge hadi baadaye.”
Alipomaliza kuahirisha, wabunge wa upinzani walibaki ndani na kufanya kikao cha dakika chache, huku wabunge wa CCM wakitoka na moja kwa moja kwenda kukutana kwenye Ukumbi wa Pius Msekwa.
 Lissu azungumzia sakata
Akizungumza kwa niaba ya wabunge wa upinzani, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu aliwaambia waandishi wa habari kuwa miswada hiyo ni migumu na kuipitisha kwa haraka wakati nchi haiko kwenye machafuko, haitawezekana.
“Muswada mmoja una vifungu zaidi ya 300 wakati vipengele vya kurekebisha ni zaidi ya 1,000, hata mimi mwanasheria ninahitaji miezi zaidi ya mitatu kumaliza kazi hiyo. Sasa, haraka hii ni ya nini?” alihoji Lissu.

Lissu alisema kwa vyovyote vile hawatakubali kwani wamebaini kuwa kuna shinikizo ndani ya Serikali kulazimisha kuipitisha miswada hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni