TANGAZO

TANGAZO

Jumamosi, 6 Juni 2015



HISTORIA YAKE
Dk Willibrod Slaa ni Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Slaa alizaliwa Oktoba 29, 1948 kijijini Kwermusi, Wilaya ya Mbulu (Oktoba atafikisha umri wa miaka 67). Slaa alisoma Shule ya Msingi Kwermusi iliyoko wilayani Mbulu mwaka 1958-1961 na baadaye Shule ya Kati (Middle School) ya Karatu kati ya mwaka 1962-1965
.
Baada ya darasa la nne, Dk Slaa alijiunga na Seminari ya Dung’unyi mkoani Singida mwaka 1966-1969 na kusoma sekondari, kisha akaendelea na masomo ya juu ya sekondari katika Seminari ya Itaga mkoani Tabora mwaka 1970 na 1971, alikohitimu kidato cha sita.
Alipomaliza kidato cha sita katika Seminari ya Itaga alikuwa amekwishafanya maamuzi ya kufanya utumishi wa kanisa. Alijiunga na Seminari ya Kibosho mwaka 1972-1973 na kupata stashahada ya Falsafa iliyompa sifa ya kudahiliwa na Seminari Kuu ya Kipalapala iliyoko Tabora kati ya mwaka 1974 na 1977 na alipata fursa ya kubobea zaidi katika masomo ya falsafa na theolojia, huku pia akisoma Stashahada ya Theolojia katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.
Dk Slaa alianza kuwa kiongozi tangu alipokuwa mwanafunzi pale Kipalapala ambapo alichaguliwa kuwa Rais wa Wanafunzi, mapadri nilioongea nao wanasema alikuwa mmoja wa viongozi wazuri sana kupata kuongoza Kipalapala.
Baada ya safari ndefu ya kuusaka “utumishi wa Mungu” Slaa alipadirishwa (alipewa upadri rasmi) mwaka 1977 na baada ya utumishi wa miaka michache alijiunga na Chuo Kikuu cha Pontifical Urbaniana nchini Italia akisomea udaktari wa Sheria za Kanisa maarufu kama J.C.D. (Juris Canonici Doctor ) au I.C.D. (Iuris Canonici Doctor) kati ya mwaka 1979 na 1981. Katika mfumo wa Kanisa Katoliki, (J.C.D au I.C.D) ndiyo shahada ya juu kabisa katika masomo ya sheria ya kanisa.
Dk Slaa amefanya kazi mbalimbali katika taasisi za Kanisa Katoliki nchini Tanzania. Amewahi kuwa Msaidizi wa Askofu na Mkurugenzi wa Maendeleo katika Jimbo la Mbulu. Amewahi kuwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) kwa muda wa miaka tisa (mihula yote mitatu). TEC ndiyo chombo cha juu cha usimamizi wa mambo ya Kanisa Katoliki hapa Tanzania.
Kwa mujibu wa Profesa Kitila Mkumbo, mhadhiri mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, katika utafiti wake juu ya Dk Slaa, anasema “…Dk. Slaa anaelezwa kama Katibu Mkuu mwenye ufanisi mkubwa zaidi tangu TEC ianzishwe. Miundombinu mingi ya Kanisa Katoliki nchini ilianzishwa na kukamilishwa katika kipindi ambacho Dk Slaa alikuwa Katibu Mkuu wa TEC.”
Dk Slaa alijitoa kwenye upadri mwaka 1991. Kwa mujibu wa taarifa za maaskofu kadhaa nilioongea nao, wanasema “Dk Slaa lifanya hivyo kwa kufuata taratibu kamili ndani ya Kanisa Katoliki na aliacha yeye mwenyewe bila kushinikizwa, kufukuzwa au kupewa onyo”.Mara kadhaa Dk Slaa alipoulizwa kwa nini aliamua kuachana na upadri, amekuwa akikaririwa akisema kwamba “kuna mambo ambayo alidhani dhamira yake ilipingana nayo na akaona asingeliweza kuendelea, japokuwa anasisitiza kuwa masuala hayo ni binafsi zaidi.”
Ndani ya Chadema amewahi kushikilia wadhifa wa Makamu Mwenyekiti, kabla hajachaguliwa kuwa Katibu Mkuu katika mwaka ambao Freeman Mbowe alichaguliwa kuwa mwenyekiti na wameendelea kuongoza kwa pamoja hadi hivi sasa.
Dk Slaa ni mwandishi mzuri wa vitabu, ameandika vitabu vitatu ambavyo ni Utimilifu wa Msichana (1977), Utimilifu wa Mvulana (1977) na Expediency and Exigency Liturgical Legislation (1981). Pia, kiongozi huyu anazungumza lugha nane kwa ufasaha; Kiswahili, Kiingereza, Kilatini, Kiitaliano, Kijerumani, Kihispania, Kireno na Kifaransa.
Dk Slaa aliwahi kumuoa Rose Kamili na kuzaa naye watoto wawili, Emiliana Slaa na Linus Slaa lakini waliachana muda mfupi kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Hivi sasa anaishi na “mchumba wake” Josephine Mushumbushi na wamepata mtoto mmoja.
  KARIBU TENA THOMASS WIKESI BLOG

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni