TANGAZO

TANGAZO

Jumatatu, 18 Januari 2016

TMAA YAKAMATA MADINI YAKITOROSHWA JNIA


Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege na Usalama wa Taifa wamekamata madini yenye thamani ya jumla ya shilingi milioni 11.2 ambayo yalikuwa yakitoroshwa kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA). 

Hayo yalisemwa jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano  wa  TMAA, Mhandisi Yisambi Shiwa ambapo alieleza kuwa raia mmoja wa kigeni na mwingine wa Tanzania walikamatwa wakiwa na madini hayo bila kuwa na kibali chochote cha usafirishaji kama ambavyo Sheria ya Madini ya mwaka 2010 inavyoelekeza.

“ Raia huyu wa kigeni ambaye jina lake linahifadhiwa kwa sababu za kiuchunguzi kwani tayari ameshafunguliwa kesi mahakamani, alikuwa anasafiri kwenda mji wa Bangkok Thailand na alikamatwa akiwa na madini ya aina mbalimbali ikiwemo almasi, aquamarine, sapphire, green tourmaline, quartz na rhodolite,” alisema Mhandisi Shiwa.

 Aidha, Mhandisi Shiwa alisema kuwa katika tukio la pili mtuhumiwa mwingine raia wa Tanzania ambaye alikuwa anasafiri kwenda Ujerumani alikamatwa akiwa na madini mbalimbali ikiwemo amethyst, moonstone cabochon, rulilated quartz (cabochon), rulilated quartz(faceted), chrysoprase, green tourmaline, rubi, red garnet, green quartz, zircon na rhodolite na kufikishwa katika vyombo vya Dola.

Alisema kuwa katika kipindi cha kuanzia mwezi Julai mwaka 2015 hadi Januari 13 mwaka huu kumekuwepo na jumla ya matukio 14 ya utoroshaji madini ambapo madini yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 1.4 (zaidi ya Shilingi Bilioni 3.2) yalikamatwa na wakaguzi wa Wakala kupitia Madawati ya Ukaguzi yaliyopo katika viwanja vya ndege vya Dar es Salaam (JNIA), Kilimanjaro (KIA) na Mwanza ambapo yote yalitaifishwa na Serikali. 

Mhandisi Shiwa ametoa rai kwa Umma kujiepusha na shughuli za utoroshaji na biashara haramu ya madini kwani hatua kali zitaendelea kuchukuliwa kwa yeyote atakayebainika au kukamatwa akijihusisha na shughuli hizo ikiwemo kutaifisha madini yaliyokamatwa.

Vilevile Mhandisi Shiwa alisema kuwa  Serikali kupitia  Wizara ya Nishati na Madini inatoa motisha kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa kwa Kamishna wa Madini ama Wakala za utoroshaji/magendo na biashara haramu ya madini ambazo zitawezesha ukamataji wa madini, atazawadiwa fedha taslimu ambazo ni asilimia 5 ya thamani ya madini yatakayokamatwa na kunadiwa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni