TANGAZO

TANGAZO

Jumanne, 29 Desemba 2015

Serikali yashtukia vifaa tiba asili, mbadala


Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Tiba Asili na
 Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Tiba Asili na Tiba Mbadala, Dk Edmund Kayombo akizungumza na wandishi wa habari kuhusu kutotambuliwa kwa mkutano wa waganga wa tiba mbadala uliofanyika juzi.
PICHA NA :MWANANCHI COMMUNICATION.

Dar es Salaam. Serikali imesema ina taarifa za kuingizwa kwa mashine za kuchukulia vipimo bila ya kusajiliwa na kusisitiza kuwa itaweka bayana msimamo wake baada ya siku 14 ilizotoa kwa matabibu wa tiba mbadala kuwasilisha taarifa za huduma zao.
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu pia amesema jana kuwa Serikali itaendelea kuzuia matangazo ya tiba asili na mbadala yasiyokuwa na kibali ili kudhibiti taarifa zinazoweza kusababisha madhara kwa umma.
Tamko hilo la Serikali linatokana na mvutano ulioibuka baada ya Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamisi Kigwangalla kupiga marufuku matangazo ya waganga wa tiba mbadala ambao wamekuwa wakinunua muda kwenye vituo vya redio na televisheni na kupigia debe kliniki zao kuwa zinatimu magonjwa sugu.
Uamuzi huo wa Dk Kigwangalla ulipingwa vikali na waganga hao waliokutana jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, wakidai kuwa sheria inawaruhusu kujitangaza.
Mvutano huo umeibuka wakati gazeti la The Citizen likifichua kifaa cha kielektroniki ambacho kimekuwa kikitumiwa na baadhi ya waganga wa tiba mbadala kufanyia uchunguzi wagonjwa na kutoa majibu yenye taarifa nyingi za mwili katika muda usiozidi dakika mbili.
Jana Waziri Mwalimu alisema kumekuwapo na uingizaji wa vifaa tiba hivyo bila ya kuvisajili na kwamba Serikali itachukua hatua.
Alisema sheria inataka kila kifaa cha tiba mbadala kinachoingizwa nchini, kisajiliwe kabla ya kuanza kutumika. “Jana nimemsikia mtu anatibu matatizo yote ya uzazi, nikajiuliza inawezekana vipi,” alisema Waziri Mwalimu.
Moja ya vifaa hivyo ni Quantum Magnetic Analyser, ambayo watengenezaji wanasema inaweza kuchukua taarifa nyingi za mwili ndani ya dakika mbili na kutoa majibu, ambayo hutumiwa na waganga hao kumshawishi mgonjwa kuwa ana matatizo sugu ya kiafya na hivyo anahitaji tiba mbadala.
Uchunguzi unaofanywa na kifaa hicho ambao haumsababishii mgonjwa maumivu wakati wa kuchunguzwa, unatiliwa shaka na wataalamu mbalimbali kuhusu usahihi wa taarifa zake.
Kuhusu matangazo ya kwenye televisheni na redio, alisema Serikali haina ugomvi na waganga wa tiba mbadala, akisisitiza kuwa iko tayari kukutana nao kujadili tamko lake kuhusu matangazo yao kwa lengo la kuboresha huduma kwa wateja wao.
“Naomba niweke wazi kwamba tiba asili na mbadala ni sehemu ya utoaji wa huduma za afya katika nchi yetu. Tunazitambua na kuzithamini,” alisema.
“Lakini tamko la wizara linabaki kuwa la Serikali kwa sababu kuna baadhi ya watoa tiba kwa kiasi kikubwa wanakiuka taratibu.”
Alisema licha ya zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania nchini kutegemea tiba hizo, kuna changamoto katika utoaji wake. Alisema sheria na kanuni zinataka tabibu ajisajili, kusajili kituo chake cha kutoa huduma au taarifa, dawa, vifaa tiba anavyovitumia na matangazo.
Alisema kanuni ya 10 ya sheria hiyo inasema hakuna tangazo lolote litakalotolewa kuhamasisha tiba hizo kwenda kwa umma isipokuwa limeidhinishwa na baraza hilo, hivyo tamko la wizara ni sahihi.
Baraza lalonga
Kwa upande wake, Baraza la Tiba Asili na Mbadala liliunga mkono tamko hilo la kuzuia matangazo na kuagiza anayetaka kutangaza huduma yake, lazima apitie kwao ili kupata kibali.
Kaimu mkurugenzi wake, Mboni Bakari alisema licha ya kutolewa vibali kwa baadhi ya matabibu wanaotoa matangazo yao kupitia vyombo vya habari, wamekuwa wakikiuka makubaliano wanayopewa.
Mwenyekiti wa baraza hilo, Dk Edmund Kayombo alisema: “Tunaomba matabibu wawe watulivu na shirikisho na baraza kwa kushirikiana na wizara ya afya kwa ujumla tunaendelea na vikao na wiki hii tunatarajia kutoa tamko. Kikubwa watupe ushirikiano na kuonyesha utii wa sheria.”
Shirikisho lanena
Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Tiba Asili na Mbadala Tanzania (Shivyatiata), Abdalrahman Lutenga alisema agizo la Serikali ni la kisheria na siyo jipya kwa sababu sheria inaeleza matangazo yote lazima yapitie baraza hilo kuhakikiwa.    

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni